Friday, July 22, 2011

Aisha Madinda apagawisha wapenzi wa Extra Bongo, aonyesha kwamba yeye bado ni mkali katika kunengua.

Mnenguaji mpya wa bendi ya Extra Bongo 'Next Level', imesababisha wapenzi wa bendi hiyo kushindwa kujizuia na kuwafanya wainuke na kumbeba juu-juu kwenye onyesho lililofanyika katika ukumbi wa Mzalendo Pub, Dar es Salaam.
Onyesho hilo lilikuwa ni mwendelezo wa maonyesho ya utambulisho wa mnenguaji huyo aliyejiunga na bendi hiyo akitokea Twanga Pepeta ambapo amekuwa akionyesho umahiri wake wa kusakata muziki wa dansi.
Utambulisho wake ulianza Jumatano ya Julai 20 katika ukumbi wa Masai uliopo Ilala na kisha kufuatiwa na mwingine katika yukumbi wa Mzalendo Pub uliosababisha mashabiki washindwe kujizuia na kumbeba juu kwa furaha.
Awali kabla ya tukio hilo, Aisha akiwa na wanenguaji wenzake walicheza shoo ya pamoja ambapo licha ya kutoonekana jukwaani kwa miezi mingi, alikuwa mwepesi, mwelevu na mjanja wa kwenda sambamba na wenzake.
Baada ya shoo ya pamoja aliachiwa nafasi yake kuamsha 'midadi' ya wapenzi wa Extra Bongo waliofurika kwenye ukumbi huo ambao 'walivamia' jukwaa na kumbeba juu kwa juu huku wakimtuza kuonyesha kuwa wameridhika na kiwango chake.
Kabla ya yote hayo, ilianza shoo kali ya wanenguaji wa wanne wa kiume walioshambulia jukwaa wakati kibao cha 'Mjini Mipango' kikipigwa, huku kikiendelea kupigwa ndipo Aisha alipopanda jukwaani kuonyesha uwezo wake.
Kama ilivyo kawaida, kabla ya mnenguaji huyo kupanda jukwaani, mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki alimwita Aisha ambapo alitumia dakika sita kucheza kabla ya wapenzi kuweweseka na kuvamia jukwaa na kumbeba juu-juu.
Baadaye wapenzi hao walimshusha ndipo aliendelea kuonyesha kuwa bado ana uwezo mkubwa wa kushambulia jukwaa kwa kiwango cha juu licha ya ukweli kwamba alikuwa nje ya jukwaa kwa kipindi kirefu akipigania afya yake.
Alipomaliza kazi yake, Aisha alijikuta akiondoka na kitita cha fedha alizotuzwa ingawa haikufahamika mara moja kwamba fedha zilikuwa ni kiasi gani.
Alipopewa nafasi ya kutoa maoni ya jinsi alivyopokelewa, Aisha alisema amefarijika kwa mwitikio wa mashabiki wengi waliojitokeza kwenye onyesho hilo na kwamba hakutegemea kupata mapokezi makubwa kwenye maonyesho mengine.

No comments:

Post a Comment