Thursday, July 7, 2011

Wazee wa Ngwasuma waja na Usiku wa Tende, Haluwa

BENDI ya FM Academia kwa kushirikiana na kampuni ya Afrika Kabisa Entertainment (ake), wanatarajia kufanya maalum lililopewa jina la Usiku wa wa Tende na Haluwa linalolenga kutambulisha nyimbo mpya za albamu ya pili.
Kwa mujibu wa msemaji wa bendi hiyo, Kelvin Mkinga, onyesho hilo litafanyika Ijumaa Julai 8 katika ukumbi wa burudani wa Vaticna City Hotel Sinza, jijini Dar es Salaam.
Katika onyesho hilo, bendi hiyo inatarajia kutambulisha baadhi ya nyimbo zikiwemo za Fataki, Chuki ya Nini na Ndoa Bandia ambazo zimekuwa zikisikika kwenye maonyesho mbalimbali ya bendi hiyo inayojiita Wazee wa Ngwasuma.
"Kampuni ya Afrika Kabisa Entertainment (ake) imetusaidia kuandaa onyesho hili ambalo limepewa jina la Usiku wa Tende Haluwa ambalo litafanyika katika ukumbi wa Vatican Sinza," alisema Mkinga.
FM Academia ni moja ya bendi zenye mashabiki wengi ambayo kila Jumamosi hutoa burudani katika ukumbi wa Kijiji cha Makumbusho na kisha Jumapili humalizia wikiendi kwenye bonanza katika ukumbi wa New Msasani Club.
Bendi hiyo imeendelea kujiimarisha ambapo sasa ina waimbaji wawili wa kike ambao ni Joyce Musiba 'Mpongo Love' na Sarah Andembwisye Mwangyombo 'Belabeloo' ambao wanashirikiana kwa karibu kufanya kazi kwenye bendi hiyo.

No comments:

Post a Comment